Donald Trump: Mexico watalipia ukuta '100%'

Donald Trump mjini Phoenix

Mgombea urais wa chama cha Republican nchini Marekani Donald Trump amesisitiza kwamba Mexico italipia ukuta utakaojengwa mpakani kuzuia raia wake kuingia Marekani asilimia 100 iwapo atashinda urais.
Ameambia umati uliomshangilia sana katika jimbo la Arizona kwamba atahakikisha ulinzi mpakani.
Kwenye hotuba muhimu kuhusu sera yake ya uhamiaji, Bw Trump pia hakufutilia mbali uwezekano kwamba mamilioni ya wahamiaji walioingia Marekani kinyume cha sheria watafurushwa iwapo ataingia mamlakani.
Saa chache awali, alikuwa amekutana na Rais wa Mexico Enrique Pena Nieto lakini akasema hawakuzungumzia ufadhili wa ujenzi wa ukuta huo.
Rais Pena Nieto baadaye alisisitiza kwamba alimwambia Trump kuwa Mexico haitalipia ujenzi huo.
Kumekuwa na uvumi kwamba huenda mgombea huyo wa Republican akaamua kuachana na mpango wake wa kuwafurusha karibu wahamiaji 11 milioni walio Marekani kinyume cha sheria.
Kwenye hotuba mjini Phoenix, alitoa ishara za kukanganya kuhusu hilo.
Amesema hatima yao si suala muhimu sana na badala yake akasema kuwafurusha 'wahalifu kutoka nje' ndilo suala la kipaumbele kwake.
"Tutamchukulia kila anayeishi au kukaa humu nchini kwa heshima anayostahili," amesema.
Lakini baadaye akaonekana kusisitiza msimamo wake mkali alipoongeza: "Kila mtu aliyeingia Marekani kinyume cha sheria anafaa kufurushwa. Hii ndiyo maana ya kuwa na sheria."
Bw Trump amesema ni haki kwa Marekani kuchagua wahamiaji ambao "tunafikiri wana nafasi ya juu zaidi ya kuishi, kufanikiwa na kutupenda".
Akifafanua, amesema "utathmini wake" wa kuamua wanaofaa kuruhusiwa kuingia Marekani ungekuwa na kifalsafa kwa wahamiaji wanaotaka kuingia Marekani.
"Wanaotaka kuingia Marekani wataulizwa maoni yao kuhusu mauaji, heshima kwa wanawake na wapenzi wa jinsia moja, na makundi ya wachache, na msimamo wao kuhusu Uislamu wa itikadi kali," amesema.
Supporters in Phoenix
Previous
Next Post »